Print Sermon

Kusudi la tovuti hii ni kuandaa makala ya mahubiri na mahubiri ya video bila malipo kwa Wachungaji na Wanamisheni duniani kote, hasa katika Ulimwengu wa Tatu, sehemu ambazo kuna uchache ama ukosefu wa vyuo vya theolojia au shule za Bibilia.

Makala ya mahubiri haya na video ufikia kompyuta 1,500,000 katika zaidi ya nchi 221 kila mwaka kupitia tovuti www.sermonsfortheworld.com. Mamia ya watu wengine hutazama video kupitia You Tube, lakini wao huondoka kutoka YouTube na kuingia katika tovuti yetu. YouTube huwaelekeza watu katika tovuti yetu. Makala ya mahubiri haya yanatolewa kwa lugha 46 kwa kompyuta takriban 120,000 kila mwezi. Makala ya mahubiri haya hayana hatimiliki, hivyo wahubiri wanaweza kuyatumia bila idhini yetu. Tafadhali bonyeza hapa ili ujue jinsi unavyoweza kutuma mchango wako kila mwezi ili utusaidie katika kazi hii kuu ya kueneza Injili kote ulimwenguni.

Kila unapomwandikia Dkt. Hymers kila wakati mjulishe nchi unayoishi, la sivyo hawezi kukujibu. Barua pepe ya Dkt. Hymers ni rlhymersjr@sbcglobal.net.




MUNGU ANAPOIONA DAMU

WHEN GOD SEES THE BLOOD
(Swahili)

na Dkt. R. L. Hymers, Jr.

Mahubiri yaliyohubiriwa katika Baptist Tabernacle kule Los Angeles
Siku ya Bwana Jioni ya, Agosti 27, 2017
A sermon preached at the Baptist Tabernacle of Los Angeles
Lord’s Day Evening, August 27, 2017

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu”
(Kutoka 12:13).


Waebrania walishuka Misri wakati wa njaa. Mwanzo walipokelewa kwa heshima kwa sababu Yusufu, mwana wa Yakobo, alikuwa mtawala chini ya Farao. Wana wa Israeli walifanikiwa na kuongezeka, lakini kulitokea Farao ambaye hakumjua Yusufu. Alipatwa na woga kwamba hesabu ya Waebrania ilikuwa inaongezeka kwa haraka na wangeweza kuteka nchi. Na hivyo akawafanya kuwa watumwa. Waebrania walimlilia Mungu katika maombi, na akamtuma Musa kuwakomboa. Lakini Farao alikuwa mkali na mkatili. Hakuwaachilia watu wa Mungu waende. Na hivyo Mungu akaleta mapigo tisa katika Misri. Kila mara walipopata pigo, Musa alienda mbele za Farao na kusema, “BWANA, Mungu wa Waebrania asema hivi, Wape watu wangu ruhusa waende.” Lakini Farao hakusikiliza. Moyo wake ulikuwa mgumu. Na ukafika wakati wa Mungu kuleta pigo la kumi.

“BWANA akamwambia Musa, Liko pigo moja bado, nitakaloleta juu ya Farao na juu ya Misri; baadaye atawapa ninyi ruhusa mtoke huku…” (Kutoka 11:1).

Na Musa akaenda mbele za Farao tena, na kusema,

“BWANA asema hivi, kama usiku wa manane mimi nitatoka nipite kati ya Misri, na wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri watakufa…Maana nitapita kati ya nchi ya Misri usiku huo, nami nitawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misrit” (Kutoka 11:4-5; 12:12).

Lakini Mungu hakutaka watu wake waadhibiwe. Alimwambia Musa kwamba kila jamii wamchukue mwana-kondoo wamchinje.

“Nao watatwaa baadhi ya damu yake na kuitia katika miimo miwili na katika kizingiti cha juu, katika zile nyumba…” (Kutoka 12:7).

Sasa simama na usome Kutoka 12:12-13 kwa sauti.

“Maana nitapita kati ya nchi ya Misri usiku huo, nami nitawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri, wa mwanadamu na wa mnyama; nami nitafanya hukumu juu ya miungu yote ya Misri; Mimi ndimi BWANA. Na ile damu itakuwa ishara kwenu katika zile nyumba mtakazokuwamo; nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu, lisiwapate pigo lolote likawaharibu, nitakapoipiga nchi ya Misri” (Kutoka 12:12-13).

Kwa karibu miaka 1,500 Wayahudi walisherehekea Pasaka. Walikila chakula muhimu cha mwana-kondoo na mkate usiotiwa chachu na kusoma kifungu hiki cha Maandiko wakati wa Pasaka, walipokuwa wakikumbuka kukombolewa kutoka utumwani wa Misri. Jina “Pasaka” linatoka katika hili andiko letu,

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

Nataka ufikirie kuhusu hili andiko kwa njia tatu. Kwanza, maana ya Damu. Pili, Mafanikio ya Damu. Na, tatu, matumizi ya Damu.

I. Kwanza, maana ya Damu.

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu.”

Je, andiko hili lina lolote kutuhusu leo? Ndio, limejaa maana, kwa sababu damu iliyomwagika katika Pasaka ya kwanza ilikuwa kielelezo cha Damu iliyomwagwa na Yesu – katika Pasaka. Ee ndio, Yesu alisulubishwa katika sherehe ya Pasaka.

“Wanafunzi wake wakamwambia, Ni wapi utakapo tuende tukuandalie uile Pasaka?” (Marko 14:12).

Walienda katika chumba cha juu kula chakula na kusoma hili andiko, Kutoka 12:13,

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

Kwanza Yesu aliwapa mkate usiotiwa chachu.

“Akatwaa kikombe, akashukuru, akawapa....Akawaambia, Hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi” (Marko 14:23-24).

Kristo alikuwa anawaonyesha ya kwamba damu iliyokuwa katika miimo katika Kutoka 12:13 ilikuwa mfano wa Damu ya agano jipya, ambayo aliimwaga Msalabani siku iliyofuatia.

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

Haikuzungumzia kila damu. Ilizungumzia kuhusu Damu ya

“Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu” (Yohana 1:29).

Damu iliyotiwa katika miimo ilielekeza na kuwa mfano wa Damu inayokomboa wenye dhamb kutoka kwa maangamizi, na kuwaweka katika

“kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe” (Mdo 20:28).

Unaweza kuuliza kwa nini Damu hii ina nguvu kiasi hiki. Spurgeon alisema,

Ikiwa Kristo alikuwa mwanadamu…hakungekuwa na nguvu ya kuokoa katika damu yake; lakini Kristo alikuwa “Mungu kikamilifu;” damu Yesu aliyomwaga ilikuwa damu kama ya Mungu. Ilikuwa damu ya mwanadamu, kwa sababu alikuwa mwanadamu kama sisi; lakini uungu ulikuwa umeunganika na ubinadamu, hivyo damu ilipata nguvu kutokana na hilo…ajabu ya milele isiyo na mwisho, kwamba Mungu amekuwa mwanadamu afe. Ee! tunapofikiria kwamba Kristo ndiye aliyeumba dunia, na kwamba ulimwengu umeshikiliwa mabegani mwake, hatuwezi kuwa na mshangao kwamba kifo chake kina uwezo wa kukomboa, na kwamba damu yake inatakaza dhambi… Kwa sababu yeye ni Mungu, “ana uwezo kabisa wa kuokoa, wote wanaokuja kwa Mungu kupitia yeye.” Damu yake ndiyo damu inayokuwezesha kuepuka hasira na ghadhabu ya Mungu (C. H. Spurgeon, “Damu,” Mimbari katika Barabara ya New Park, Chapicho la Pilgrim, 1981 chapa ya pili, sehemu ya V, uk. 27-28).

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

Damu iliyokuwa katika miimo ya mlango ilikuwa mfano wa Damu ya Mungu-mtu, Kristo Yesu.

“Kwa maana Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo” (I Wakorintho 5:7).

Na hiyo ndiyo maana ya Damu!

II. Pili, mafanikio ya Damu.

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

“Nitapita juu yenu.” Hakuna hukumu itakayowafikia. Hakuna laana itakayowapata – ikiwa uko na hiyo Damu.

“Kwa kuwa BWANA atapita ili awapige hao Wamisri; na hapo atakapoiona hiyo damu katika kizingiti cha juu, na katika ile miimo miwili, BWANA atapita juu ya mlango, wala hatamwacha mwenye kuharibu aingie nyumbani mwenu kuwapiga ninyi” (Kutoka 12:23).

Hakuna hukumu kutoka kwa Mungu inayoweza kumpata mwanamume au mwanamke aliye na Damu.

“Nanyi twaeni tawi la hisopo, mkalichovye katika ile damu iliyo bakulini na kukipiga kizingiti cha juu, na miimo miwili ya mlango, kwa hiyo damu iliyo katika bakuli…” (Kutoka 12:22).

Damu katika kizingiti – mwimo wa juu. Damu katika kila upande, katika miimo ya kado. Damu iliyo chini ya bakuli. Iliyo juu. Iliyo chini. Iliyo kila upande. Kitendo hiki kilikuwa kielekezi cha msalaba wa Kristo!

Tazama, kutoka kichwani Mwake, mikononi Mwake, miguuni Mwake,
   Huzuni iliyo changanyika na upendo ilitiririka;
Je, upendo wa namna hii na huzuni zilikutana,
   Ama miiba kutengeneza taji nzuri hivyo?
(“Ninapouangalia Msalaba wa Ajabu” na Isaac Watts, 1674-1748).

“Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha na dhahabu…bali kwa damu ya dhamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na mawaa, yaani ya Kristo” (I Petro 1:18-19).

Martin Luther anauliza,

Ni ipi sasa, iliyo hazina ambapo tunakombolewa? Si dhahabu au fedha iaribikayo lakini ni Damu ya thamani ya Kristo, Mwana wa Mungu. Thamani hii ni ghali na bora kwamba hakuna akili au fikira ya mwanadamu inaweza kuifahamu, hata ingawa tone moja tu ya hii damu isiyo na hatia ingetosha kwa ajili ya dhambi ya ulimwengu. Walakini Baba alitaka kutoa kwa wingi na utele neema yake juu yetu na akakubali ukombozi wetu umgharimu kwa njia kuu kwamba alimkubali Kristo, Mwana Wake, kumwaga damu yake yote kwa ajili yetu na hivyo akatukirimia hazina yote (Luther, Maelezo kuhusu I Petro 1:18-19).

Damu ya Kristo ilitiririka chini kama matone ya jasho pale Gethsemane. Damu yake ilitiririka alipochubuliwa kwa kupigwa mijeledi katika sebule ya Pilato. Taji ya miiba ilichubua uso wake na Damu ikatiririka kwa macho yake. Misumari ilitoboa mikono na miguu yake, na Damu ikatiririka kutoka Msalabani. Halafu, askari akamchoma umbavuni,

“Na mara ikatoka damu na maji” (Yohana 19:34).

“[Mungu] alimruhusu Kristo, Mwana Wake, kumwaga damu yake yote kwa ajili yetu na hivyo kutukirimia hazina yote” (Luther, ibid.).

Na

“damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi zote” (I Yohana 1:7).

Dhambi yote inaoshwa na Damu ya Kristo Yesu! Dhambi yote! Hakuna dhambi iliyo kuu kiasi cha kwamba haiwezi kuoshwa na Damu yake! Hakuna dhambi ambayo Damu haiwezi kuiosha. Inatoa pepo saba za Mariamu Magdalene. Inaondoa wazimu wa yule aliyekuwa amepagawa na pepo. Inaweza kuponya vidonda vibaya vya ukoma. Hakuna ugonjwa wa kiroho haiwezi kuponya. Hakuna jambo lisilowezekana kwa Damu, haijalishi linachukiza au potovu kiasi gani, kwa sababu ni Damu ya Kristo inayotoshelesha yote.

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

Na hiyo inaonyesha mafanikio ya Damu!

III. Tatu, matumizi ya damu.

Kama mwana-kondoo angekuwa amenyongwa au kupewa sumu, mwenye kuharibu angewahukumu wazaliwa wa kwanza wa kila jamii. Kama mwana-kondoo engeuawa na kufungwa katika mwimo, mwenye kuharibu angeingia na awapige. Wale wanaosema hakuna Damu wafahamu hilo. Haikuwa kifo cha mwana-kondoo pekee, lakini damu ya mwana-kondoo iliyoleta utofauti. Ni Kweli, mwana-kondoo alikuwa afe, na bado Mungu akasema,

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

Lakini damu iliyo baki ndani ya bakuli haikuzuia hukumu. Ni lazima itumike. Chukua tawi la hisopo

“mkalichovye katika ile damu... na kukipiga kizingiti cha juu, na miimo miwili ya mlango” (Kutoka 12:22).

Damu ni lazima itumike la sivyo haitakuwa na mafanikio. Ee, mwenye dhambi, chukua Damu ya Kristo! Huoshwe dhambi zako na Damu ya Yesu!

“Kristo Yesu: ambaye Mungu amekwisha kumweka awe upatanisho kwa njia ya imani katika damu yake” (Warumi 3:24-25).

Ni jambo la ajabu kuona Biblia ya NASV imelitafsiri hili andiko vizivyo, katika tafsiri wanayoiita tafsiri halisi! Na bado Biblia ya NIV imelitafsiri vyema, “kwa njia ya imani kupitia damu yake.” Nachukia kurudi nyuma na kwenda mbele. Na hii ndiyo sababu nimeshikamana na tafsiri ya zamani iliyoaminifu ya KJV, ambayo imetafsiriwa kwa njia halisi na inaaminika.

“Kwa njia ya imani katika damu yake.”

Kiini cha imani ni Damu ya Kristo. Hivyo ndivyo unavyofanya mapatano. Hivyo ndivyo Damu inavyotumika juu yako – “kwa imani kupitia damu yake.”

“Loo hapana,” madhehebu mengine wanaweza kusema, “haujaokolewa kwa imani kupitia Damu yake!” Barabara, ningetaka kujua jinsi unavyoweza kuokolewa bila damu yake! “Vyema, ikiwa mtu atategemea Damu, anaweza angamia.” Haiwezekani! Haiwezi kuwa hivyo! Mungu angekuwa si wa kweli kwake yeye mwenyewe ikiwa atakuachilia uangamie unapoitegemea Damu ya Kristo!

“kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi” ... kwa msamaha wa dhambi (Mathayo 26:28).

Kuna watu wengi ambao awahisi Damu ikiwa juu yao. Lakini hilo alijalishi, kwa sababu andiko letu halisemi ya kwamba ni wewe unayehitaji kuiona Damu. Hapana! Linasema,

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

Mungu ndiye anayehitaji kuiona Damu. Mungu ndiye pekee anayehitaji kuiona au kuihisi Damu inayokutakaza dhambi zote. Andiko halisemi “utakapoiona damu.” Andiko halisemi ya kwamba ni lazima uelewe mambo yote kuhusu utakazo kupitia Damu ya Kristo. Andiko linasema, “nitakapoiona.” Imani yako inaweza kuwa si kubwa sana. Lakini unapokuja kwa Yesu na kuamini Damu yake, Mungu ataona hilo. Ndiye tu anayehusika. Na

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

Waebrania hawangeiona damu. Walikuwa ndani ya nyumba zao. Hawangeweza kuona ni nini ilikuwa kwa kizingiti na miimo. Lakini Mungu aliiona hiyo Damu pale. Hilo tu ndilo sharti ambalo linalohitajika kwa wokovu wa mwenye dhambi – Mungu anapoiona Damu juu yako, si wewe unapoiona. Halafu uje kwa Mungu kwa njia ya maombi na useme, “Bwana, niokoe kwa ajili ya Damu ya Kristo”. Siwezi kuiona vyema kama ninavyostahili, lakini Bwana, unaiona, na umesema,

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

“Bwana, unaiona Damu. Unaona ya kwamba nimeamini nguvu za Damu zinazookoa. Nisamehe na unitakaze kwa ajili ya Damu ya Kristo pekee.” Fanya hilo kuwa ombi na shauku ya moyo wako na utaoshwa uwe msafi kwa Damu ya Yesu hivi karibuni!


UNAPOMWANDIKIA DKT. HYMERS NI LAZIMA UMWAMBIE UNAANDIKA KUTOKA NCHI GANI AU HATAJIBU BARUA PEPE YAKO. Ikiwa mahubiri haya yatakubariki tuma barua pepe kwa Dkt. Hymers na umwambie lakini kila mara mjulishe unaandika kutoka nchi gani. Barua pepe ya Dkt. Hymers ni rlhymersjr@sbcglobal.net (bonyeza hapa). Unaweza kumwandikia Dkt. Hymers kwa lugha yeyote, lakini andika kwa kingereza ikiwa unaweza. Ikiwa unataka kumwandikia Dkt. Hymers kupitia posta, anwani yake ni S.L.P. 15308, Los Angeles, CA 90015. Unaweza kumupigia simu kupitia nambari hii (818)352-0452.

(MWISHO WA MAHUBIRI)
Unaweza soma mahubiri ya Dkt. Hymers kila wiki kwa Tovuti
hii www.sermonsfortheworld.com.
Bonyeza hapa kwa “Mahubiri kwa Kiswahili.”

Maandishi ya mahubiri haya hayana hatimiliki. Unaweza kuyatumia bila ruhusa ya
Dr. Hymers. Hata hivyo, mahubiri yote ya video ya Dkt. Hymers, na mahubiri mengine yote
ya video kutoka kwa kanisa yetu, yako na hatimiliki na yanaweza tumiwa tu kwa kuuliza ruhusa.

Wimbo ulioimbwa kabla ya mahubiri:
“Ninapoiona Damu” (na John Foote, Karne ya19).


MWONGOZO WA

MUNGU ANAPOIONA DAMU

WHEN I SEE THE BLOOD

na Dkt. R. L. Hymers, Jr.

“Nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu” (Kutoka 12:13).

(Kutoka 11:1, 4-5; 12:12, 7)

I.   Kwanza, maana ya Damu, Marko 14:12, 23-24; Yohana 1:29;
Mdo 20:28; I Wakorintho 5:7.

II.  Pili, mafanikio ya Damu, Kutoka 12:23, 22;
I Petro 1:18-19; Yohana 19:34; I Yohana 1:7.

III. Tatu, matumizi ya Damu, Warumi 3:24-25; Mathayo 26:28.